Mbio za kusaka Kombe la Dunia zitaanza leo kati ya Russia Vs Saudi Arabia

Mechi hiyo itaanza saa kumi na mbili jioni saa za Afrika Mashariki.
Michuano hiyo itashirikisha mataifa 32, wakiwemo mabingwa watetezi Ujerumani, na itakuwa na mechi 64 zitakazochezwa katika kipindi cha siku 32.
Fainali itachezwa 15 Julai.
Fainali za sasa za Kombe la Dunia ambazo ni za 21 zitachezwa katika viwanja 12 katika miji 11 nchini Urusi, ambayo inapatikana eneo la upana wa maili zaidi 1,800.
Kutokana na hili, kutakuwa na tofauti kubwa katika wakati mechi zinachezwa.
Ujerumani, waliowashinda Argentina katika fainali ya Kombe la Dunia 2014, wanapania kuwa taifa la kwanza kushinda kombe hilo mtawalia kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1962.
Brazil nao wanatafuta kuweka rekodi nyingine kwa kushinda kombe hilo kwa mara ya sita.
Michuano hiyo ya mwezi mmoja inatarajiwa kuwavutia mashabiki nusu milioni kwenda Urusi na kote duniani inatarajiwa kutazamwa na watu zaidi ya bilioni tatu.
Kuna makundi manane, kila kundi likiwa na timu nne. Timu mbili ambazo zitamaliza juu kwenye kundi ndizo zitakazosonga hadi hatua ya 16 bora.
Fainali itachezewa katika uwanja wa Luzhniki ambao hutoshea mashabiki 81,000 mnamo 15 Julai.
Nani atashinda Kombe la Dunia?
Mabingwa watetezi Ujerumani, mabingwa mara tano Brazil, washindi wa Euro 2016 Ureno, waliomaliza wa pili 2014 Argentina, Ubelgiji, Poland na washindi wa mwaka 1998 Ufaransa ni timu nane ambazo zilikuwa kwenye chungu wakati wa kufanywa kwa droo.
Wote wanapigiwa upatu kushinda.
Wenyeji Urusi walikuwepo kwenye chungu pia ingawa ndio walioorodheshwa wa chini zaidi kwa viwango vya soka kwa kufuata orodha ya Fifa ya kila mwezi, ambapo kwa sasa wameorodheshwa wa 70.
England, ambao wameshinda mechi moja pekee kati ya nane walizocheza karibuni zaidi Kombe la Dunia hawakuwa kwenye chungu, sawa na mabingwa wa mwaka 2010 Uhispania.
Ujerumani wamefika angalau nusu fainali katika kila michuano minne iliyochezwa karibuni, na baada ya kuwa timu pekee kufuzu kwa kushinda mechi zote Ulaya, wanatarajiwa kutoa ushindani mkali.
Wamo Kundi F na Mexico, Sweden na Korea Kusini.
"Ujerumani watawindwa kama ambavyo haijawahi kutokea awali," anaamini kocha wao Joachim Low.
"Ni sisi pekee, kama mabingwa watetezi, tuna kitu cha kupoteza."
Brazil ndiyo nchi pekee ambayo imeshiriki michuano hiyo bila kukosa tangu ilipoanzishwa lakini hawajashinda tangu 2002.
Mara ya mwisho kwao kushinda wakiwa barani Ulaya ilikuwa ni mwaka 1958.
Hata hivyo, Brazil wana matumaini, hasa kupitia nyota wao Neymar aliyeweka rekodi ya dunia kwa kununuliwa £200m alipohamia Paris Saint Germain ya Ufaransa kutoka Barcelona Agosti 2017.
Alikuwa ameumia mapema mwaka huu lakini amepona na kucheza mechi kadha za kirafiki za kimataifa akiwa na Brazil, na kufunga.
Uhispania wana mabingwa kadha wa Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya kutoka Real Madrid kwenye kikosi chao na watatakakutwaa kombe hilo tena kama walivyofanya miaka minane iliyopita, na waliposhinda ubingwa Ulaya 2008 na 2012.
Upande mwingine, Cristiano Ronaldo naye atakuwa anatafuta medali yake ya kwanza ya kushinda Kombe la Dunia baada ya kuwasaidia Ureno kushinda Euro 2016, Lionel Messi naye akitumai kwamba atashinda kombe lake la kwanza kuu akiwa na Argentina.
Ufaransa wana kikosi kichanga na kilichojaa wachezaji wa kusisimua, akiwemo mshambuliaji wa miaka 19 Kylian Mbappe.
Aidha, wana wachezaji nyota kutoka Ligi ya Premia wakiwemo kipa wa Tottenham Hugo Lloris, kiungo wa kati wa Manchester United Paul Pogba na mshambuliaji wa Chelsea Olivier Giroud.
Waamuzi kusaidiwa na VAR
Teknolojia ya kuwasaidia waamuzi (VAR) itatumiwa kwa mara ya kwanza Kombe la Dunia wakati huu.
Teknolojia hiyo itatumiwa kuwasaidia waamuzi kuepuka makosa ambayo yanaweza kusaidia kuamua mshindi wa mechi, hasa wakati wa kukubali goli, mikwaju ya penalti au kadi nyekundu.
VAR tayari imekuwa ikijaribiwa England, Ujerumani na Italia.
Teknolojia hiyo ilitumiwa mara ya kwanza katika Kombe la Dunia la Klabu Desemba 2016 na ikajaribiwa katika Kombe la Mashirikisho 2017
Usalama
Urusi inapanga kuandaa michuano ya kufana baada ya kuwashinda England, Uhispania na Ureno, na Uholanzi na Ubelgiji, katika kupigania haki za kuwa mwenyeji.
Ni mara ya kwanza Urusi kuandaa michuano hiyo.
Mashabiki karibu 10,000 wa England wanatarajiwa kusafiri Urusi, lakini baadhi huenda wasisafiri kutokana na uhasama uliozidi kati ya nchi hizo mbili na wasiwasi pia kuhusu usalama.
Makabiliano yalitokea kati ya mashabiki wa Urusi na England mataifa hayo yalipokutana Marseille wakati wa Euro 2016.
Ghasia pia zilizuka kati ya mashabiki wa England, Urusi na Ufaransa.
No comments